Tabora/Manyoni/Dar.
 Mgombea urais kwa tiketi ya Chadema anayeungwa mkono na Umoja wa Katiba
 ya Wananchi (Ukawa), Edward Lowassa jana alizua sintofahamu baada ya 
kusema; “CCM oyee”, kauli iliyowafanya wananchi hao kukaa kimya na 
walipoona akicheka waliitikia “oyeee” huku nao wakicheka na 
kumshangilia.
Ingawa ilitokana na ulimi kuteleza, yeye mwenyewe alisema alitamka neno 
CCM kama utani ili kubaini ni wananchi wangapi wanaokishabikia chama 
hicho kati ya waliojitokeza uwanjani hapo kumsikiliza wakati tayari 
amekwishaeleza jinsi chama hicho tawala kilivyoshindwa kuliletea taifa 
maendeleo.
Msindai kama Lowassa
Wakati Lowassa akieleza kwamba alisema hayo kwa utani aliyekuwa 
Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Singida, Mgana Msindai aliyekihama chama hicho
 na kujiunga na Chadema, alitoa mpya baada ya kukiombea kura chama chake
 hicho cha zamani badala ya Ukawa kwenye mkutano wa hadhara.
Msindai alitoa mpya hiyo juzi jioni wakati akizungumza kwenye mkutano wa
 uzinduzi wa kampeni Jimbo la Manyoni Magharibi na Mashariki uliofanyika
 Manyoni mjini kwa tiketi ya Ukawa.
Baada ya kuwanadi wagombea wa nafasi za ubunge na udiwani wa majimbo 
hayo, Msindai ambaye pia alikuwa mwenyekiti wa wenyeviti wa CCM 
Tanzania, aliwaomba wakazi wa Manyoni akisema:
“Mpeni kura Lowassa ni mchapakazi na mwadilifu, anauchukia umaskini 
ataikomboa nchi yetu na kura zote za Rais, wabunge na madiwani wapeni 
wagombea wa Chama cha Mapinduzi.”
Baada ya tamko hilo, uwanja ulilipuka kwa kelele na minong’ono ndipo 
kiongozi mmoja aliponyanyuka na kwenda alipokuwa Msindai ameketi na ni 
kama alimwambia: “Hapa ni Ukawa si CCM.”
Alipopata maelekezo hayo, Msindai alisimama na kusema: “Ninaomba radhi, 
unajua koo limekauka, hebu kwanza naomba mnipe maji nipooze koo.”
Alipoletewa maji na kuyanywa, aliendelea kuomba radhi na kusema: “Ndugu 
zangu, ulimi uliteleza... si mnajua tumetoka huko hivi karibuni Uccm 
haujatutoka sawasawa,” alisema na kuamsha kicheko kwa mashabiki 
waliokuwa wakimsikiliza.
Akizungumza kwa simu jana, Msindai alikiri kuombea kura wagombea wa CCM 
kwenye mkutano wa Ukawa lakini alisema kuwa ulimi uliteleza na kwamba 
aliomba radhi na watu walimwelewa.
Hata hivyo, Msindai alikazia kusema kuwa Watanzania wanataka mabadiliko 
kwani hata mgombea wa CCM, Dk John Magufuli katika hotuba zake amekuwa 
akisema anataka kuona Tanzania ikibadilika.
“Watanzania watabadilika ikiwa Dk Magufuli atatimua watu wote kwenye 
mfumo wa utawala na kuleta mabadiliko ya kweli, lakini kama watu 
watabakia walewale, watamwangusha,” alisema Msindai.
Alipoulizwa utayari wa Watanzania kubadilika, Msindai alisema Ukawa 
ndiyo watakaoleta mabadiliko ya kweli kwa kuwa watawaondosha watu wote 
na kuleta watu wapya kwa ajili ya kufanya kazi,” alisema.
Alisema CCM ya sasa siyo ile ya (Julius) Nyerere na imebadilika na 
haitumikii tena wananchi na kwamba, Dk Magufuli ni mwenye hasira hivyo 
anakosa sifa.
Mmoja wa makada wa Chadema Mkoa wa Singida, Paschal Mlaki alieleza 
kushangazwa na kuteleza kwa Msindai akisema ana wasiwasi na waliokuja 
kwenye chama hicho. “Mimi ni kada wa Chadema hapa Singida, hakuna 
asiyenijua, ukweli hili limetukwaza wengi... hivi inaingia akilini kweli
 uko mkutano wa Ukawa ukatangaza CCM?
“Watu wanatumia gharama zao kufanya maandalizi, wanataka kupata vitu vya Ukawa halafu anakuja kututangazia haya!”
Chanzo: Mwananchi
 
 
 
 
 




 
No comments :
Post a Comment